DC KONGWA ATEMBELEA ENEO LA MAEGESHO YA MAGARI KIBAIGWA
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari – Kongwa DC
Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon Mayeka ametembelea na kukagua mradi wa ujenzi wa eneo la maegesho ya magari lililopo mamlaka ya mji mdogo Kibaigwa na kuongea na wafanyabiashara wa eneo hilo.
Mhe. Mayeka amefanya ziara hiyo Novemba 19 kufuatia malalamiko ya wafanyabiashara katika eneo la Kibaigwa kupinga magari yasiegeshwe katika eneo jipya la maegesho yanayojengwa kwa kisingizio cha kukosa wateja katika biashara zao ambazo awali zilikuwa zinanufaishwa na abiria wa magari hayo yaliyokuwa yakiegeshwa katikati ya mji kwenye maeneo yasiyo rasmi.
Nae Diwani wa Kata ya Kibaigwa Mhe. Daudi Kweka amefafanua kuwa licha ya wananchi hao kulalamikia maegesho hayo lakini wameomba kupunguzwa kwa vigingi vilivyojengwa pembezoni mwa barabara kwani vimekuwa vikihatarisha maisha ya waendesha pikipiki na waendesha baskeli.
Akiongea mbele ya Mhe. Mkuu wa Wilaya, Mhandisi Elisony Edward Mweladzi wakala wa barabara Tanzania TANROADS Mkoa wa Dodoma amesema kuwa wafanyabiashara hao walifikisha malalamiko yao kwa uongozi wa Serikali ya Kata ya Kibaigwa wakitaka maegesho ya magari yasihame kutoka yalipokuwa yakiegeshwa awali.
Akijibu hoja hizo mbele ya wafanyabiashara hao Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka amesema ujenzi wa maegesho hayo ni muhimu ili kuondoa adha wanayopata Wananchi kutokana na msongamano wa magari makubwa katikati ya mji hivyo wafanyabiashara wasiangalie maslahi yao binafsi waangalie na watumiaji wengine wa barabara.
Aidha katika hatua hiyo Mhe. Mayeka amemuagiza Mhandisi wa TANROADS Mkoa wa Dodoma kupunguza vigingi vya pembezoni mwa barabara kwa kuzingatia usalama wa wananchi na kulinda miundombinu ya barabara hiyo kwani lengo la Serikali ni kuondoa msongamano na si kukwamisha biashara za wananchi hivyo ni vyema wananchi wakafuata utaratibu uliowekwa.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.