DC. MAYEKA “USALAMA KATIKA WILAYA YA KONGWA NI JUKUMU LA KILA MMOJA”
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari kongwa DC
Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji pamoja na Watendaji wa Kata na Vijiji wamekumbushwa kuwa jukumu la usalama wa wananchi katika Wilaya ya Kongwa ni la kila mmoja katika eneo analofanyia kazi. Hayo yamesema leo na Mkuu wa Wilaya ya Kongwa na Mwenyekiti wa kamati ya Ulinzi na usalama Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka S. Mayeka katika kikao kilichokutanisha viongozi wa serikali za Mitaa pamoja na VEO’S na WEO’S na kamati ya ulinzi na usalama ya Wilaya.
DC Mayeka amewaasa viongozi kuwa makini kuwatambua wageni kutoka nchi Jirani ambao wamekuwa wakiingia katika nchi ya Tanzania bila vibali na kujichanganya na wazawa na wengi wao wamekuwa wakifanya uhalifu hivyo viongozi wa Serikali za Mitaa wawe makini kutambua kila mkazi anayeishi eneo husika na wageni wanaolala katika nyumba za wageni.
Aidha DC Mayeka ameshauri kuwa mgambo wahusishwe katika vikao vya usalama katika vijiji maana wamepatiwa mafunzo ambayo yanawapa uwezo wa kutambua viashiria vya uhalifu na wana mafunzo ya njia za kuanza kutatua changamoto hizo jambo ambalo litamaliza changamoto za vitendo vya kiuhalifu.
Mambo mengine yaliyoongelewa kwenye kikao ni pamoja na swala la uharibifu wa mazingira ikiwemo ukataji miti holela unaofanyika katika maeneo mbalimbali ya Wilaya pamoja na wizi wa mifugo na mazao na viongozi wameaswa wasiwaonee haya wahalifu na watoe taarifa zenye ukweli na Ushahidi ili wahalifu wote washughulikiwe kwa mujibu wa sheria.
Akifunga kikao hicho, DC Mayeka amewaasa Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji pamoja na Watendaji wa Kata na Vijiji kuvunja makundi yaliyokuwepo katika kipindi cha uchaguzi na kampeni na kuhakikisha kuwa kila kiongozi anafanya kazi kwa kushirikiana na mwingine bila kujali itikadi ya chama ili kusudi wananchi wa Kongwa wapate maendeleo.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.