DED KONGWA “USIMAMIZI WA MIRADI NI MUHIMU KWA UREJESHWAJI WA MIKOPO 10%”
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari Kongwa DC
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa Dkt. Omary Nkullo ametoa msisitizo kwa Maafisa Maendeleo ya Jamii Wilaya ya Kongwa kuongeza kasi ya ufuatiliaji na usimamizi wa miradi inayofanywa na wanavikundi waliopatiwa mikopo ya fedha za 10% ya wanawake vijana na watu wenye ulemavu ili kuwa na urejeshwaji mzuri wa fedha hizo.
Dkt. Nkullo ameyasema hayo januari 8 2026 alipokuwa katika kikao cha robo ya pili cha divisheni ya maendeleo ya jamii cha kujadili taarifa mbalimbali zikiwemo za ufatiliaji na tathmini na mikopo chechefu ambapo ameeleza kuwa kuna haja ya divisheni kutafuta mtaalam wa masuala ya usimamizi wa miradi ili kuwanoa maafisa hao ili waweze kuwa na uelewa wa kufatilia vizuri miradi inayofanywa na wanavikundi na kuleta tija kwa wanavikundi na Halmashauri.
“taarifa za wanavikundi bado hazijitoshelezi, watembeleeni mara kwa mara na mtoe taarifa kila mwezi mjue hali za miradi yao makazi yao ya kudumu au kama wamehama mjue changamoto zao pia msipike tu taarifa wafatilieni” alisema Dkt. Nkullo.
Licha ya kukemea suala la rushwa wakati wa kupitisha vikundi vinavyotakiwa kukopeshwa lakini pia Dkt. Nkullo amewataka Maafisa Maendeleo ya Jamii kuwa na lunga rafiki na kupeleka tabasamu kwa wananchi kwa kuwapokea na kuwahudumia vizuri wakati wote.
Akiongea katika kikao hicho Mkuu wa Diviheni ya Maendeleo ya Jamii Wilaya ya Kongwa Bi. Paskalina Duwe amesema kuna changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo katika kusimamia miradi ikiwemo wanavikundi wengi kujitegemea katika uendeshaji wa shughuli zao bila kuwa na wataalam husika kwa ajili ya kuwashauri mfano Maafisa Ugani na Biashara hivyo divisheni imeandaa kikao cha pamoja na wataalam mbalimbali ili kuwashirikisha suala hilo.
“suala la mikopo linagusa watu wengi Mkurugenzi, Mkuu wa Wilaya na Mhe. Rais pia hivyo sisi Maafisa Maendeleo ya Jamii tumepewa jukumu kuhakikisha fedha hizi zinatumiwa kama ilivyopangwa wananchi wananufaika na Halmashauri yetu ifanye vizuri katika utoaji na urejeshwaji wa fedha hizi za 10%.
Kwa upande wake Afisa Maendeleo ya Jamii Kata ya Lenjulu Bw. Michael Emmanuel amesema kuwa suala la usafiri ni changamoto inayokwamisha kazi ya ufatiliaji wa vikundi hususani kwa Kata zilizopo pembezoni kama Lenjulu Chitego Chiwe na Zoissa hivyo wanaomba wapatiwe pikipiki.
Aidha bw. Emmanuel amefafanua kuwa changamoto ya kuweka akiba kwa vikundi ni kutokana na umbali kutoka Kata au Vijiji walivyopo kwenda benki, licha ya baadhi ya vikundi kuweka akiba kupitia kwa mawakala wa benki waliopo karibu na maeneo yao na baadhi yao kukopeshana ili kuzitunza na kuzalisha.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.