WAGANGA WA TIBA ASILI NA TIBA MBADALA WAIBUENI WAGONJWA KWA KUWAPA RUFAA
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari - Kongwa DC
Waganga wa tiba asili na tiba mbadala Wilayani Kongwa wametakiwa kuwaibua wagonjwa wanaofika katika vituo vyao vya kutolea tiba kwa kuwapa rufaa kwenda Hospitali endapo watashindwa kuwahudumia kwa utaalamu wao.
Hayo yameelezwa na Dkt Melkizedeki Kongola Mratibu wa Malaria Wilaya ya Kongwa alipomwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kongwa katika hafla ya ugawaji wa leseni za baraza la tiba asili na tiba mbadala iliyofanyika katika Kata ya Ngomai ambapo amesema kuwa utoaji wa rufaa hizo utasaidia kuokoa maisha ya wagaonjwa.
Dkt. Kongola amewataka waganga wote wajitahidi kupata leseni ili waweze kufanya kazi kihalali bila kusumbuliwa na vyombo vya dola na kupunguza malalamiko katika jamii juu ya utendaji kazi wao.
Licha ya kupongeza Baraza la tiba asili na tiba mbadala TAMESO T (Traditional and Alternative Medicine Society of Tanzania) lakini pia Dkt. Kongola amewasihi waganga hao kufanya kazi kwa kufuata taratibu, kanuni na sheria za kuendesha tiba asili Nchini Tanzania.
Nae Mratibu wa Huduma za jamii Wilaya ya ongwa Bi Rehema Chitemasi akizungumza kwa niaba ya Mganga Mkuu Wilaya ya Kongwa amesema kuwa tiba asili ni mwanzo wa tiba zote na ugawaji wa leseni hizi ni kuhakikisha Wilaya ya Kongwa haina waganga wa tiba asili ambao hawafuati utaratibu.
Akisoma Risala ya mbele ya mgeni rasmi Katibu wa wagaga wa tiba asili na tiba mbadala Wilaya ya Kongwa Bw. Lukas Mlipu amesema kuwa lengo la chama cha TAMESO T ni kuwaweka waganga pamoja kutambua nafasi zao, kutoa elimu ya kuepuka ramli chonganishi, usafi maeneo ya kazi na kueleza faida za kutoa rufaa kwa wagonjwa inapobidi.
Licha ya kuipongeza Serikali kwa kuweka vituo vya tiba asili katika baadhi ya hospitali Nchini lakini pia Bw. Mlipu ameiomba Serikali kuwachukulia hatua waganga wote wasio kuwa na leseni wanaofanya kazi kinyume cha sheria na taratibu.
Sambamba na hayo kwa upande wao waganga wa tiba asili tiba mbadala wamewaomba viongozi wa Serikali kuwaonya watu wanaotumia majukwaa yao kutangaza vibaya kazi zinazofanywa na waganga wa tiba asili kwani hali hiyo inaweza kupelekea uvunjifu wa amani na jamii kutowaamini.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.