WALIMU WAKUU WAHIMIZWA UTEKELEZAJI WA MAJUKUMU YAO
Na Bernadetha Mwakilabi
Habari Kongwa DC
Walimu Wakuu wa Shule za Msingi na Waratibu Elimu Kata Wilayani Kongwa wamehimizwa kufanya tathmini ya utekelezaji wa majukumu yao mara kwa mara ili waweze kufikia malengo ya ufaulu bora na wa juu kwa matokeo ya mtihani wa Darasa la saba 2026.
Hayo yameelezwa na Katibu Tawala Wilaya ya Kongwa Bi. Sozi Ngate alipomwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Mayeka Simon Mayeka katika kikao cha Walimu Wakuu wa Shule za Msingi Kongwa cha kufanya tathmini ya matokeo ya Mwaka 2025 na kuweka mikakati imara ya ufundishaji ili kufikia lengo la ufaulu wa 100% kwa Mwaka 2026.
"ikiwa lengo letu ni kufikia 100% tukiamua tunaweza tuendelee kujipanga kuongeza ufaulu wa watoto kwa kufanya tathmini ya kazi zenu na kuongeza kasi ya uandikishaji wa wanafunzi wa awali na darasa la kwanza ili tuwe na watoto wengi wanaokwenda Sekondari" alisema Ngate.
Licha ya Bi. Ngate kusisitiza upendo baina ya Walimu, Walimu Wakuu na Waratibu Elimu Kata lakini pia amewasihi kuendelea kusimamia Miradi ya ujenzi inayoendelea katika shule zao na kuwashirikisha wazazi katika suala la upungufu wa Madawati ili waweze kuwasaidia kwani nao ni wadau wa elimu.
Sambamba na hayo nae Afisa Elimu Awali na Msingi Wilaya ya Kongwa Mwl. Margareth Temu amesema kuwa katika Mwaka 2025 Shule za Msingi 118 zilizofanya mtihani wa darasa la saba, shule 88 zilipata ufaulu wa 100% na kufanya Wilaya kushika nafasi ya pili Kimkoa kwa kuwa na wastani wa 98.99% hili ni jambo la kijivuania japo kuwa kumekuwa na changamoto katika masomo ya Kiingereza na Hisabati.
Aidha Mwl. Temu ameongeza kuwa kwa kuwa sera yao ni kuhakikisha wanafunzi wote wanaoanza darasa la kwanza wanafika kidato cha nne hivyo ameahidi kuwarudisha Shule Wanafunzi 60 waliofeli mtihani wa darasa la saba Mwaka 2025 ili nao waweze kutimiza ndoto zao.
Katika hatua hiyo nae Afisa Utumishi Bi. Zubeda Nunda akiongea kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kongwa licha ya kuwapongeza kwa ufaulu mzuri 2025 lakini pia amewakumbusha walimu kujaza taarifa zao katika mfumo wa Pepmis, kuongeza ushirikiano na ofisi yake na kuacha mikopo chechefu badala yake wakope kwa malengo maalum.
Kwa upande wake Mdhibiti Mkuu Ubora wa Shule Wilaya ya Kongwa Dkt. Yohana M Chikuni amewakumbusha walimu wakuu na waratibu kuimarisha ushirikiano kwa kutoa taarifa juu ya changamoto walizonazo kuwa wakweli na wawazi kutanguliza mbele maslahi ya elimu na kuwa wasiri pale inapobidi.
Nae Afisa Maadili na Nidhamu kutoka tume ya utumishi wa walimu Wilaya ya Kongwa Ndg. Oscar Mpechi amewahimiza walimu kuvaa mavazi ya staha wanayotakiawa kuvaa watumishi wa umma na kuacha ulevi na utoro kwani mambo hayo yanashusha hadi ya mtumishi.
Akiongea katika kikao hicho mwenyekiti wa Walimu Wakuu Wilaya ya Kongwa Mwl. Loishooki Mollel amemshukuru Afisa Elimu Awali na Msingi Wilaya kwa kuwa na mawasiliano thabiti baina yake na walimu hali inayorahisisha utekelezaji wa majukumu na kuahidi kufanya vizuri katika matokeo ya mtihani wa darasa la saba Mwaka 2026 kutokana na mikakati imara ya ufundishaji waliyojiwekea.
Ofisi ya Mkurugenzi Mtendaji Wilaya
Anuani ya Posta: S.L.P 57 Kongwa, Dodoma
Simu ya Mezani: +255 26 2370031
Simu ya Mkononi: +255 713399349
Barua pepe : ded@kongwadc.go.tz
Copyright ©2022 Kongwa District Council . All rights reserved.